19/11/2025
Waziri Mkuu Mstaafu, Mhe. Kassim Majaliwa Kassim, mapema leo ametembelea wagonjwa waliolazwa katika wodi mbalimbali za Taasisi ya Saratani Ocean Road (ORCI) na kutoa salamu za faraja pamoja na pongezi kwa watumishi wote wanaojituma kuwahudumia wagonjwa.
Akiwa katika wodi ya wagonjwa mahututi (ICU), Mhe. Majaliwa amepongeza kazi kubwa inayofanywa na madaktari, wauguzi na wataalamu wengine kwa kujitoa kwao kila siku kuokoa maisha.
Katika ziara hiyo, Mhe. Majaliwa amesisitiza umuhimu wa kuendeleza moyo wa huruma, utu na umakini kwa wagonjwa, akisema kuwa huduma nzuri ndiyo nguzo ya matarajio ya wananchi wanaotegemea ORCI kwa matibabu ya saratani.
Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi wa ORCI, Dkt. Crispin Kahesa, amemshukuru Mhe. Majaliwa kwa kutenga muda wa kutembelea wagonjwa na watumishi, akibainisha kuwa ujio wake umeleta faraja kubwa na kuwapa hamasa wagonjwa pamoja na watumishi wanaohudumu katika mazingira yenye changamoto.
Dkt. Kahesa amesema kuwa, ziara hiyo imethibitisha kwa vitendo dhamira ya viongozi wa taifa katika kusimamia afya ya wananchi.
Katika hatua nyingine Dkt. Kahesa ametoa shukrani za dhati kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kuendelea kuiwezesha ORCI kupitia vifaa tiba vya kisasa, maboresho ya miundombinu na kuimarisha upatikanaji wa huduma za kisasa za matibabu ya saratani.
Dkt. Kahesa amesema mashine za kisasa zilizopatikana zimeongeza ufanisi wa matibabu na kupunguza muda wa kungojea huduma.
Kwa kumalizia, Dkt. Kahesa amesisitiza kuwa mafanikio ya ORCI yanatokana na juhudi za watumishi wanaofanya kazi kwa kujituma usiku na mchana, pamoja na serikali kuamua kuwawezesha.
Dkt. Kahesa ameahidi kuwa taasisi itaendelea kuimarisha ubora wa huduma na kushirikiana na serikali pamoja na wadau mbalimbali kuhakikisha wananchi wanapata matibabu bora, salama na yenye ufanisi.