23/02/2026
Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) Yaweka Jiwe la Msingi la Mageuzi ya Taasisi ya Saratani Ocean Road (ORCI)
Safari ya Mageuzi kuelekea Kituo cha Ubora Barani Afrika
Tarehe 23 Februari 2026 itaendelea kukumbukwa k**a siku ya kihistoria katika safari ya mageuzi ya Taasisi ya Saratani Ocean Road (ORCI). Mchango wa shilingi milioni 361.5 uliotolewa na Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) si tu msaada wa kifedha, bali ni uwekezaji wa kimkakati unaoashiria imani, matumaini na dira ya pamoja ya kuiwezesha ORCI kufikia hadhi ya Kituo cha Ubora (Centre of Excellence) katika huduma za saratani barani Afrika.
Kwa zaidi ya miaka 30 tangu kuanzishwa kwake, ORCI imeendelea kupiga hatua kubwa katika utoaji wa huduma za uchunguzi, tiba ya mionzi, kemotherapi na huduma shirikishi. Hata hivyo, kukosekana kwa chumba cha upasuaji ndani ya taasisi kulibaki kuwa pengo kubwa katika mnyororo wa huduma za saratani. Wagonjwa walilazimika kufanyiwa uchunguzi ORCI, kisha kwenda hospitali nyingine kwa ajili ya upasuaji, na baadaye kurejea ORCI kuendelea na matibabu. Hali hii ilisababisha usumbufu, ucheleweshaji wa matibabu, gharama za ziada na wakati mwingine athari za kiafya kwa wagonjwa, hususan kina mama na makundi mengine yenye uhitaji mkubwa.
Ujenzi wa jengo jipya la upasuaji unaondoa changamoto hiyo ya muda mrefu na kuifanya ORCI kuwa One Stop Centre kituo jumuishi kinachotoa huduma kamili chini ya paa moja. Hii si hatua ndogo; ni mapinduzi ya kimfumo yanayoweka misingi ya huduma za kimultidisciplinary, ambapo wataalamu wa upasuaji, tiba ya mionzi, tiba ya dawa (chemotherapy), uchunguzi wa kimaabara na huduma za uangalizi wa karibu watafanya kazi kwa pamoja kwa manufaa ya mgonjwa.
Kwa mtazamo wa kitaalamu, uwepo wa huduma ya upasuaji ndani ya ORCI utaongeza ufanisi wa mipango ya matibabu (treatment planning), kuimarisha ushirikiano wa kitabibu (tumor boards) na kupunguza muda wa kusubiri huduma. Wagonjwa watanufaika na mwendelezo wa matibabu usiokatika, jambo linaloongeza nafasi ya mafanikio ya tiba na kuboresha ubora wa maisha yao.