27/02/2026
WAZIRI WA AFYA MHE. MOHAMED MCHENGERWA AFANYA ZIARA YA KIMKAKATI HOSPITALI YA RUFAA YA MKOA AMANA
Waziri wa Afya, Mohamed Mchengerwa, leo Februari 27, 2026, amefanya ziara ya kimkakati katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Amana kwa lengo la kukagua utolewaji wa huduma za afya pamoja na maendeleo ya uboreshaji wa miundombinu ya hospitali hiyo.
Katika ziara hiyo, Mhe. Mchengerwa ameambatana na Katibu Mkuu Dkt. Seif Shekalaghe pamoja na menejimenti ya Wizara ya Afya, ambapo alikagua hali ya upatikanaji wa huduma, kusikiliza changamoto zinazowakabili watumishi na wagonjwa, na kueleza mikakati madhubuti ya serikali katika kuimarisha ubora na ufanisi wa huduma za afya kwa wananchi.
Aidha, Waziri Mchengerwa amesisitiza umuhimu wa uwajibikaji, nidhamu ya kazi na matumizi sahihi ya rasilimali zilizotengwa na Serikali ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora, salama na kwa wakati.
Sambamba na hayo Mhe. Mchengerwa Amesema Serikali itaendelea kuwekeza katika ununuzi wa vifaa tiba vya kisasa, kuongeza wataalamu wa afya na kuboresha mazingira ya kutolea huduma ili kukidhi mahitaji ya wananchi wanaotegemea hospitali hiyo na vituo vingine vya afya nchini.