22/04/2026
MOI KUWA KITUO CHA KWANZA CHA UMAHIRI MATIBABU YA MGONGO AFRIKA YA MASHARIKI NA KATI
Na Abdallah Nassoro - MOI
Taasisi ya Tiba ya Mifupa na Ubongo Muhimbili (MOI) imekuwa ya kwanza katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kati kutoa matibabu ya kisasa ya mgongo bila upasuaji.
Mkurugenzi Mtendaji wa MOI Mhe: Balozi Dkt. Mpoki Ulisubisya amebainisha hayo leo Aprili, 22, 2026 wakati akiongea na waandishi wa habari baada ya taasisi hiyo kufanikiwa kutoa matibabu hayo ya kisasa kwa wagonjwa 20.
“Kwa muda mrefu tumekuwa tukishirikiana na chuo kikuu cha afya cha Weill Cornell cha nchini Marekani katika ubadilishanaji wa afua mbalimbali za matibabu ya ubongo, mgongo na mishipa ya fahamu katika nyanja za upasuaji, lakini leo hii tumekuja na afua mpya kabisa na ya kisasa duniani, nayo ni matibabu ya mgongo bila kupasua” amesema Dkt. Mpoki na kuongeza
“Kwa afua hii MOI imekuwa taasisi ya kwanza Afrika Mashariki na Kati kutoa matibabu haya na inakwenda kuwa kituo mahiri cha kufundishia wataalam katika ukanda huu, habari hii ni faraja kwa wagonjwa wote wenye matatizo ya mgongo ambao hawatalazimika kufanyiwa upasuaji”
Kwa upande wake Mratibu wa mafunzo hayo Daktari bingwa wa upasuaji wa ubongo, mgongo na mishipa ya fahamu Dkt. Hamisi Shabani amesema matibabu ya mgongo bila kufanya upasuaji ni mbinu mpya na ya kisasa inayotoa nafuu kwa wagonjwa.
“Matibabu haya ni tofauti na yale ya mazoezi tiba (Physiotherapia), hii ni teknolojia ya kisasa na ni fahari kwetu MOI kuwa taasisi ya kwanza kutoa matibabu ya aina hii, na tutakuwa taasisi ya kwanza Afrika, wagonjwa hawa 20 watakuwa mashuhuda wa matibabu haya” amesema Dkt. Shabani
Mkurugenzi wa huduma za matibabu ya mgongo kutoka Chuo Kikuu cha Weill Cornell cha nchini Marekani, Prof. Roger Hartl amesema ushirkiano wa miaka 15 na MOI umekuwa wa mafanikio makubwa na kwamba utolewaji wa afua hiyo mpya ya matibabu ya mgongo bila kupasua ni kielelezo cha ufanisi.