27/01/2026
ELIMU YA BIMA YA AFYA KWA WOTE NI ENDELEVU – DKT. MFANGA
Mganga Mkuu wa Mkoa wa Njombe, Juma Mfanga amesema kuwa Elimu ya Bima ya Afya kwa wote inapaswa kuwa endelevu ili kuleta matokeo yaliyokusudiwa na serikali.
Akizungumza jana jioni Januari 26, katika Kikao chake na Menejimenti ya Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Njombe, amesema kuwa ipo haja kubwa ya Uongozi wa Hospitali kupitia wakuu wa Idara na vitengo, kuwafikishia watumishi walio chini yao Elimu ya Bima ya Afya kwa wote, ili kuendana na kasi ya Utekelezaji wa mpango huo ambao umeanza rasmi hapo jana.
Miongoni mwa sababu zilizotajwa kuchangia uanzishwaji wa Bima ya Afya kwa wote ni pamoja na kuwezesha malengo ya kisera, k**a vile kupunguza vifo vitokanavyo na uzazi yaani vifo vya mama na mtoto, kutengeneza uwiano katika utoaji huduma kwa kujumuisha makundi maalumu k**a vile Watoto, wajawazito, wasio na uwezo, na wazee;Ujumuishaji wa huduma za magonjwa yanayochangia/kusababisha vifo na madhara makubwa ya kiafya kwa haraka.
Menejimenti ya Njombe RRH ilipitishwa katika maeneo mbalimbali ikiwemo utekelezaji wa Sheria ya Bima ya Afya kwa wote,namna mifumo ya TEHAMA itakavyotakiwa kufanya kazi kuanzia Ngazi ya Afya ya Msingi hadi Taifa kwa kusisitiza kuwa mifumo hiyo lazima iboreshwe na ikiwezekana uwepo mfumo mmoja ambao utasaidia kusomana kwa Taarifa kuanzia Zahanati hadi Hospitali ya Taifa, ikiwa ni agizo la Waziri wa Afya, Mhe. Mohamed Mchengerwa,kuimarisha upatikanaji wa huduma bora za Afya; mfano upatikanaji wa dawa za kutosha, kuimarisha mifumo ya Tiba mtandao (Telemedicine) pamoja na utaratibu wa Rufaa.
Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Njombe, Gilbert Kwesi amesisitiza wakuu wa Idara na Vitengo kushusha elimu hiyo kwa watumishi waliopo chini yao, pamoja na kuagiza Mratibu wa Mafunzo na Tafiti kuandaa kipindi ambacho kitasaidia kutoa elimu kwa watumishi wote kuhusu Bima ya Afya kwa wote.
Kupitia Bima ya Afya kwa wote Kaya yenye watu wasiozidi sita (6) wataweza kufaidika na huduma ya matibabu kwa gharama ya 150,000/= kwa mwaka.