
16/07/2025
MKURUGENZI WA HOSPITALI YA KIBONG’OTO AITEMBELEA NJOMBE RRH
Mkurugenzi wa Hospitali Maalum ya Tiba ya Magonjwa Ambukizi kibong’oto, Dkt. Leonard Subi leo hii Julai 16 ametembelea Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Njombe na kukutana na Menejimenti ya Hospitali ambapo amepata wasaa wa kutembelea maeneo mbalimbali ya utoaji huduma ikiwemo Kitengo cha Uchunguzi wa Magonjwa ya Mfumo wa Chakula na Maabara.
Ziara ya Dkt. Subi, imelenga kuangalia na kutoa ushauri wa namna nzuri ya kujikinga na magonjwa ya mlipuko na magonjwa ambukizi kwa kuimarisha huduma ya utambuzi na uchunguzi wa magonjwa hayo ikiwemo ugonjwa hatari wa Kifua kikuu.
Amepongeza Uongozi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Njombe kwa kuendelea kusimamia uimara wa miundombinu ya Hospitali, ubora wa Huduma za Afya ikiwemo vipimo vya maabara , pamoja na kupata Ithibati ya Ubora wa Huduma za Maabara kutoka SADCAS.
Ameahidi kuwa Hospitali ya Kibong’oto itaendelea kushirikiana na Uongozi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Njombe ikiwemo kuwajengea Uwezo wataalamu mbalimbali wa afya katika maeneo mbalimbali ya taaluma zao hususani eneo la uchunguzi wa maabara ili kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma za Afya na utambuzi wa mapema wa magonjwa haya.
Kwa upande wake Mganga Mfawidhi, Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Njombe Dkt. Gilbert Kwesi amemshukuru Dkt. Leonard Subi na ujumbe alioambatana nao kwa ujio wake, kwa kile alichoeleza kuwa Uongozi wa Njombe RRH upo tayari kuendelea kushirikiana na Hospitali ya Kibong'oto kuimarisha afua za Kifua kikuu na magonjwa ambukizi kwa ujumla ikiwemo kutoa wataalamu wake ambao watapata nafasi ya kwenda kujengewa uwezo, kujifunza na kuongeza ujuzi, ili kuongeza ubora katika utoaji huduma.